Ugiriki: kisiwa cha Kos chazidiwa na wingi wa wahamiaji
Wahamiaji wameendelea kuwasili kwa wingi katika visiwa vya Ugirikivilio karibu na Uturuki. Hali ya wasiwasi imetanda katika kisiwa cha Kos. Kuna zaidi ya wahamiaji 7,000 katika idadi ya wakazi 30,000.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Mbele ya uwanja mdogo wa mpira wa mji wa Kos ambapo wahamiaji wametakiwa kujiandikisha mbele ya mamlaka ya kisiwa hicho ili kuweza kuendelea na safari yao, lakini hali ya kutisha na mivutano vimeanza kushuhudiwa.
Wahamiaji hao ni kutoka nchi nyingi, wengi wao ni kutoka Syria. Wote wamekua wakijaribu kuingia uwanjani, huku wakizuiliwa na polisi wa kutuliza ghasia, amearifu mwandishi wetu katika kisiwa cha Kos, Daniel Vallot. Matumaini yao: kupata ruhusa ya kuondoka Kos, ili waweze kujielekeza Athens.
Maelfu ya wahamiaji wamewasili miezi ya hivi karibuni katika bahari Aegean. Kutokana na ongezeko hilo la wahamiaji haramu, viongozi wa Ugiriki wamesema kuwa wamezidiwa na hali hiyo.
Uthibitisho kwamba hali hiyo imekua mbaya zaidi, Jumanne wiki hii, ghasia zilizuka kati ya wahamiaji katika kisiwa cha Kos. Wakiwatawanya kwa kurushiwa gesi pamoja na kupigwa fimbo, vikosi vya usalama vilijaribu kurejesha udhibiti wa hali hiyo.
Wahamiaji na wakimbizi 1,500 walikusanyika Jumanne wiki hii katika uwanja mdogo wa mpira katika kisiwa cha Kos nchini Ugiriki. Watu hao ikiwa ni pamoja na wanaume, wanawake na watoto wenye asili ya Syria wangelipaswa kujiorodhesha kwa viongozi wa kisiwa hicho wakati, kwa sababu ambazo bado hazijawekwa wazi, hali ilikua tata kwa vurugu kati ya wahamiaji.