Ugiriki yakabiliwa na majanga ya moto
Serikali ya Ugiriki imetoa ombi kwa Ulaya kuisaidia kupambana dhidi ya majanga ya moto yanayoteketeza misitu wakati huu ambapo moto umezuka mapema Ijumaa mchana wiki hii katika maeneo mawili tofauti, ikiwa ni pamoja na eneo lililo karibu na mji wa Athens na kusini mwa Peloponnese.
Imechapishwa:
Janga la kwanza la moto limetokea katika mlima Ymette, kilomita 10 kutoka katikati ya mji wa Athens, moto ambao umejitokeza mapema Ijumaa mchana na kuathiri sehemu kadhaa za msitu uliyokaribu na eneo hilo, Mkuu wa kitengo cha zima moto amesema wakati wa mkutano na waandishi wa habari.
" Maafisa 140 wa kitengo cha zima moto, magari 60, ndege saba, helikopta nne vimetengwa ili kujaribu kuzima moto huo ambao umezuka mapema Ijumaa wiki hii ", amesema Afisaa huyo.
" Watawa 50 wamehamishwa kutoka eneo wanakoishi katika mlima huo ", msemaji wa kitengo cha zima moto Nikos Tsogas amesema katika mkutano na waandishi wa habari Ijumaa alasiri wiki hii.
Katika mji wa Laconia, karibu na mji wa Neapolis, moto ulianza usiku wa Alhamisi kuamkia Ijumaa wiki hii. Nyumba tano zimeteketea kwa moto, kwa mujibu wa Nikos Tsogas. " Maafisa 120 wa kitengo cha zima moto, magari 51, ndege tatu, helikopta mbili" vimetengwa kwa kazi ya kuzima moto huo leo Ijumaa kwenye majira ya alasiri.
Matukio matatu mapya ya moto pia yameripotiwa Ijumaa mchana wiki hii katika kisiwa cha Evia karibu na mji wa Athens (ambapo ndege ilitumiwa) katika shughuli ya kuzima moto huo. Katika mji wa Malakassa kilomita 40 kaskazini mwa mji wa Athens (ndege mbili) zimetumiwa, na katika karibu na mji wa Nafplion katika jimbo la Peloponnese.
" Ugiriki imefanya maombi rasmi kwa Idara ya Ulaya inayohusika na utaratibu wa dharura ", amesema Waziri mkuu Alexis Tsipras kwa vyombo vya habari baada ya kukutana na wakuu wa kitengo cha wazima moto. Maombi haya yanalenga ndege nne maalumu kwa kuzima moto wenye nguvu unaoteketeza kwa muda mfupi misitu na mashamba.
Majanga hayo yamesababishwa na upepo mkali ambao huenda ukaendelea kupiga katika maeneo mengi nchini Ugiriki Jumamosi mwishoni mwa wiki hii, ameonya Nikos Tsogas.
Georges Harakiris, naibu meya wa wilaya ya Heliopolis, moja ya maeneo ya jirani ya Mlima Ymette, amesema majanga hayo ya moto yametokea kwa " makusudi " kwa sababu wakazi wamesikia milipuko kabla ya moto huo kuzuka. Hata hivyo polisi haijathibitisha.
Kwa upande wao, viongozi wa serikali za mitaa katika jimbo la Laconia wamebaini kwamba watu wakaazi wa vijiji kati ya vili na vinne wamehamishwa kwa tahadhari.