Iraq: mateka wa Uingereza Alan Henning auawa
Wapiganaji wa Dola la Kiislam wamekiri Ijumaa wiki hii kumuua raia wa Uingereza, Alan Henning, waliokua wakimshikilia kwa kipindi kirefu, baada ya kumteka nyara.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Wapiganaji hao wa Dola la Kiislam wamebaini kwamba mateka huyo ameuawa kwa kulipiza kisase kwa mashambulizi ya anga yanayotekelezwa na Uingereza dhidi ya ngome zao nchini Iraq.
Alan Henning, mwenye umri wa miaka 47, alikua akijitolea kwa kusaidia raia wa Syria, ambako alikotekwa nyara na kupelekwa nchini Iraq.
Mkanda wa video unaodumu dakika moja, ambao unaanza na ujumbe kwa Marekani na washirika wake dhidi ya Dola la Kiislam, umemuonesha mateka huyo akijieleza kabla ya kukatwa kichwa, kama jinsi ilivyokua kwa mateka wengine waliyouawa na wapiganaji wa Dola hilo la Kiislam.
Alan Henning amesikika akisema kwenye mkanda huo wa video kwamba anauawa kutokana na Bunge la Uingereza kupitisha uamzi wa kushambulia wapiganaji wa Dola la Kiislam nchini Iraq.
Alan Henning, kabla ya kujiunga na shirika la kihisani, alikua dereva katika mji wa Machester nchini Uingereza. Alijitolea kuwasaidi wahanga wa vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Syria, na alikua ameshafanya shughuli nyingi akiwa katika shirika la kihisani lililoundwa na jamii ya waislam nchini Uingereza. Alan Henning alitekwa nyara mwezi Desemba mwaka 2013 na watu wenye silaha.
Baada ya kutekwa kwa raia huyo wa Uingereza, serikali ya Uingereza ilijizuia kutoa taarifa zozote zinazohusiana na kutekwa nyara kwa Alan Henning kwa kuhofia kutoweka hatarini maisha ya mateka huyo.
Alan Henning ni mateka wa tano kuuawa na kundi hilo la Dola la Kiislam, baada ya mataifa ya magaharibi kuanzisha mashambulizi yao dhidi ya Dola hilo nchini Iraq na Syria.