Raia wa Ufaransa aliyekua anashikiliwa Niger aachiwa huru
Wizara ya kigeni nchini Ufaransa imesema kuwa raia wake na mwanabiashara Stephane Jullien aliyekua anashikiliwa na utawala wa Niger ameachiwa huru.
Imechapishwa:
Stephane ambaye pia alikua akiwakilisha maslahi ya Wafaransa kutoka nje katika ubalozi wa Ufaransa alikamatwa tarehe 8 Septemba baada tuu ya mapinduzi.
Uhusiano kati ya Niger na Ufaransa ulidorora haraka baada ya mapinduzi ya Julai 26, ambayo yalimwondoa madarakani rais mshirika wa Ufaransa Mohamed Bazoum.
Hata hivyo wiki zilizopita rais wa Ufaransa Emannuel Macron alisisitiza kwamba Ufaransa isingelibadilisha msimamo wake wa kuyalaani mapinduzi ya kijeshi na kuahidi kumsaidia rais aliyepinduliwa, Mohamed Bazoum, akisisitiza kwamba ndiye aliyechaguliwa kidemokrasia na kwamba alikuwa jasiri kwa kukataa kujiuzulu.
Paris, ambayo ina takriban wanajeshi 1,500 waliotumwa nchini Niger kama sehemu ya mapambano mapana ya Ufaransa dhidi ya wanajihadi katika eneo la Sahel, imemshikilia na kumuunga mkono Bazoum na kutangaza mamlaka ya baada ya mapinduzi kuwa yalikua haramu na kushinikiza kurejeshwa kwa utawala wa kiraia.
Kumekuwa na uvumi kwamba Ufaransa italazimika kujiondoa kikamilifu kijeshi kutoka Niger, huku chanzo cha wizara ya ulinzi ya Ufaransa kikisema kuwa jeshi la Ufaransa lilikuwa likifanya mazungumzo na jeshi la Niger juu ya kuwaondoa wanajeshi wake