Katibu mkuu wa UN ailaumu Urusi kwa kusitisha mkataba wa usafirishaji nafaka
Nairobi – Ni pigo kwa usalama wa chakula duniani na hasa katika nchi zenye uhitaji, haya ni matamshi ya katibu mkuu wa umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, wakati akieleza masikitiko yake baada ya Urusi kutangaza kujitoa kwenye makubaliano ya usafirishaji nafaka katika eneo la Black Sea.
Imechapishwa:
Guterres, amewaambia waandishi wa habari kuwa, kwa mara nyingine Urusi imeshindwa kuwajibika hata kwa kidogo ambacho kilikuwa msaada mkubwa kwa nchi masikini.
“Mwishowe ushiriki katika makubaliano haya ni uamuzi binafasi lakini watu wanaotaabika kila mahali na katika nchi zinazoendelea hawana cha kuchagua, mamia kwa maelfu ya watu wanakabiliwa na njaa.” alisema katibu mkuu wa UN.
Katibu mkuu wa UN kuhusu mkataba wa usafirishaji nafaka
Tayari mataifa ya Ulaya na Marekani, yamekashifu hatua ya Urusi waliyoitaja kama usaliti.
Naye rais wa Ukraine Volodymry Zelensky, amesema nchi yake iko tayari kuendelea kusafirisha nafaka licha ya Urusi kujiondoa katika mkataba uliokuwa umeratibiwa nan chi ya Uturuki na umoja wa Mataifa.
Zelensky ameikashifu Moscow kwa kile amesema ni muendelezo wa ukatili wa taifa hilo kwa nchi masikini.
“Kila mtu ana haki ya utulivu, Afrika ina haki ya utulivu, Asia ina haki ya utulivu, Ulaya ina haki ya utulivu. Kwa hiyo sote yatupasa kuzingatia suala la usalama dhidi ya ukichaa wa Urusi.” alieleza rais Zelensky.
Volodymry Zelensky, Rais wa Ukraine
Kiongozi huyo aidha alisema kwamba mkataba wa Black Sea unaweza na lazima uendelee hata kama ni bila ya Urusi na kwamba makubaliano hayo yalikuwa kati ya Uturuki na umoja wa mataifa na bado yako hai.
Ukraine inasema kwamba kile kinachohitajika kwa sasa ni kutekeleza makubaliano hayo kwa umakimini na dunia kuongeza shinikizo dhidi ya utawala wa kigaidi wa Urusi.