Ukraine : Mtu mmoja ameuawa katika shambulio la ndege zisizo na rubani
Nairobi – Kyiv imethibitisha kutokea kwa shambulio kubwa la ndege zisizo na rubani usiku kucha ambapo mtu mmoja ameripotiwa kuawaua kwenye tukio hilo ambalo limetekelezwa na wanajeshi wa Urusi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kwa mujibu wa mkuu wa utawala wa kijeshi wa Kyiv, Serhiy Popko, ametaja shambulio hilo kama "la watu wengi" kwa kutumia ndege zisizo na rubani za Shahed zilizotengenezwa na Iran ambazo zilitoka pande tofauti.
Kwa mujibu wa maofisa nchini Ukraine wa kupambana na ndege za kivita, mtu mmoja aliuawa katika tukio hilo baada ya vifusi vya ndege hizo vilivyokuwa na moto kuanguka ambapo pia watu wanne walijeruhiwa wakati wa makabiliano hayo ya angani.
Milipuko ilisikika tena katika mikoa mingine ya Ukraine, ikijumuisha Khmelnitskyi magharibi, Mykolaiv kusini na Zaporizhia kusini mashariki.
Haya yanajiri wakati huu waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov akisema kwamba hajasikia mapendekezo yoyote mapya kuhusu mpango wa mauzo ya nafaka wa Bahari Nyeusi, ambao unatamatika Jumatatu.
Makubaliano hayo yaliyosimamiwa na umoja wa mataifa na Uturuki Julai mwaka jana, yanairuhusu Ukraine kusafirisha nafaka kupitia Bahari Nyeusi hadi sehemu za dunia zinazokabiliwa na njaa, jambo limetajwa kusaidia katika suala la kukabiliana na usalama wa chakula duniani baada ya vita hivyo kusababisha mfumuko wa bei za bidhaa.
Mnamo Mei, Urusi ilikubali kuongeza mkataba huo kwa siku 60.