Biden atetea hatua yake ya kuihami Ukraine na mabomu ya kivita
Rais wa Marekani Joe Biden ametetea "uamuzi wake mgumu" wa kuipa Ukraine mabomu ya kivita, ambayo yana rekodi ya kuua raia.
Imechapishwa:
Rais alisema ilimchukua "muda kushawishika kufanya hivyo", lakini alichukua hatua kwa sababu "Ukraine inakabiliwa na uchache silaha".
Rais wa Ukraine alipongeza hatua hiyo amabyo alisema inafa lakini mashirika ya haki za binadamu na baadhi ya wanademokrasia walikosoa uamuzi huo. Urusi nayo ikilaani hatua hiyo.
Biden aliiambia CNN katika mahojiano Ijumaa kwamba alikuwa amezungumza na washirika kuhusu uamuzi huo, ambao unakuja kabla ya mkutano wa kilele wa Nato nchini Lithuania wiki ijayo.
Mabomu ya aina hiyo yamepigwa marufuku na zaidi ya nchi 120, lakini yametumiwa na Urusi na Ukraine wakati wa vita.
Mshauri wa usalama wa kitaifa Jake Sullivan alisema kwamba "wanatambua mabomu ya hayo yanaleta madhara kwa raia" kutokana na mabomu ambayo hayajalipuka.
"Hii ndiyo sababu tumeahirisha uamuzi huo kwa muda mrefu tuwezavyo."
Sullivan alisema Ukraine inaishiwa na silaha na ilihitaji kupigwa jeki huku Marekani ikiongeza uzalishaji wake wa ndani.
"Hatutaiacha Ukraine bila ulinzi wakati wowote katika kipindi hiki cha mzozo," alisema.
Wasi wasi umeibuka kuhusu mabomu madogo ambayo hayajalipuka yanaweza kukaa ardhini kwa miaka mingi na kulipuka kiholela baadaye.
Mshauri huyo aliwaambia waandishi wa habari kwamba mabomu hayo ya Marekani yanayotumwa Ukraine yalikuwa salama zaidi kuliko yale aliyosema tayari yanatumiwa na Urusi katika mzozo huo.