Guterres: Mazungumzo ya amani kati ya Urusi na Ukraine hayawezekani kwa sasa
NAIROBI – Katibu mkuu wa umoja wa mataifa, Antonio Guterres, amesema mazungumzo ya kutafuta amani kati ya Ukraine na Urusi kwa sasa hayatawezekana.
Imechapishwa:
Kauli ya Guterres imetokana na kwamba mataifa yote mawili, Ukraine na Urusi yamezama katika vita, kila pande ikiamini kwamba itavishinda vita hivyo, hivyo basi Guterres anaona kwamba kushawishi mataifa hayo mawili kuacha vita kwa sasa ni vigumu.
Hata hivyo katibu mkuu huyo kwenye mahojiano na gazeti la Spanish daily El Pais, amesema anatumai siku za usoni Ukraine na Urusi watakaa kwenye meza ya mazungumzo kutafuta amani.
Haya yanajiri wakati rais wa Urusi Vladmir Putin, katika sherehe za kuadhimisha kumalizika kwa vita vya pili vya dunia, akiashiria kwamba Urusi huenda isirejea nyuma katika uvamizi wake nchini Ukarine, na kuongeza kwamba dunia ilianzisha vita dhidi ya urusi.
Jumatatu, Mei 8, rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky, aliapa kwamba Urusi itashindwa katika uvamizi wake nchini Ukraine jinsi wapiganaji wa kinazi walivyoshindwa.
Aidha waziri wa mambo ya nje wa China, Qin Gang, anatarajiwa barani Ulaya juma hili, wakati huu China ikionekana kama mpatanishi kati ya Ukraine na Urusi.