Urusi: Mamluki wa Wagner watishia kuondoka Bakhmut Ukraine
NAIROBI – Mkuu wa mamluki wa Urusi Wagner ,Yevgeny Prigozhin, kwa mara nyengine tena hii leo Ijuma amerejelea kauli yake ya awali kwamba atawaondoa wapiganji wake katika mji wa Bakhmut mashariki mwa Ukraine.
Imechapishwa:
Ametoa matamshi haya wakati akizungumza kando na miili ya wale anaodai ni wapiganaji wake anaosema wameuawa baada ya kuishiwa risasi.
Urusi imekuwa ikijaribu kuuteka mji huo kwa miezi kadhaa ambapo kiongozi huyo ameendelea kutoa wito kwa serikali ya Moscow kuwapa wapiganaji wake silaha zaidi.
Hii sio mara ya kwanza kwa mkuu huyo wa Wagner kutoa kauli kama hiyo madai yake yakionekana kupuuzwa na serikali ya Urusi.
Katika video hiyo aliyoichapisha kwenye mtandao wa Instagram akiwaonyesha watu anaosema ni wanajeshi wake wakiwa wameuawa, Prigozhin amemlaumu waziri wa ulinzi wa Urusi Sergei Shoigu na mkuu wa wafanyakazi Valery Gerasimov kwa kusababisha vifo vya askari wake.
Aidha mkuu huyo wa Wagner katika video hiyo, anasikika akiuliza wapi silaha? “Hawa waliofariki wako hapa kusaidia na sasa wanafariki.” Ametoa matamshi haya akiwa amesimama kando na miili hiyo.
Vile vile Prigozhin ambaye ni mtu wa karibu wa rais Putin, amesikika akisema kuwa wapiganji wake wanapungukiwa asilimia 70 ya silaha akionya kuchukua hatua iwapo swala hilo halitatuliwa.
Madai haya ya Wagner yanakuja wakati huu mzozo kati ya Urusi na Marekani ukionekana kuongezeka baada ya waziri wa mambo ya kigeni wa Urusi Sergei Lavrov kuituhumu Washington kwa kuhusika katika jaribio la shambulio la ndege zisizo na rubani dhidi ya Kremlin.
Ukraine kwa upande wake imekana kuhusika na madai hayo ya Urusi, rais akisisitiza kwamba nchi yake haishambulii Moscow wala Putin bali inajikinga.
Marekani kwa upande wake imekana kuhusika na tuhuma za Urusi, Washington ikisema kwamba Kremlin inasema uongo.