Rais Zelensky: Hatutekeleza jaribio la kumuua rais Putin
NAIROBI – Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelenskiy, amekanusha nchi yake kutumia ndege zisizo na rubani kujaribu kushambulia Moscow na kumuua rais Vladmir Putin, utawala wa Kiev ukiituhumu Urusi kupanga kilichotokea.
Imechapishwa:
Kauli ya Zelensky, imekuja saa chache tangu utawala wa Moscow, udai kuwa ulidungua ndege kadhaa zisizo na rubani kutoka Ukraine, zilizojaribu kumuu rais Putin bila hata hivyo kuweka wazi ushahidi kuhusu hilo.
“Sisi hatumshambulii Putin au Moscow, sisi tunapigana ndani ya mipaka yetu, tunalinda mipaka yetu na miji yetu na hatuna silaha hata za kutosha kufanya hivyo na ndio maana hatuzitumii popote tu.” Alisema rais Zelensky.
Volodymyr Zelenskiy, Rais wa Ukraine
Katika hatua nyingine, rais Zelensky, amefanya ziara ya kushtukiza kwenye nchi ya Uholanzi, akibeba ajenda kuhusu mahakama ya ICC kuchukua hatua kwa uhalifu uliotekelezwa na Urusi nchini mwake.
Urusi imeishtumu Ukraine kwa kujaribu kutumia ndege yake isiyokuwa na rubani kwa lengo la kumuua, rais Vladimir Putin.Haya yakiwa ndio madai makubwa zaidi tangu Moscow ilipoivamia Kiev mwaka mmoja uliopita.
Madai haya yametolewa na serikali jijini Moscow na kuripotiwa na vyombo mbalimbali vya Habari vya ndani na nje ya nchi hiyo.
Hata hivyo, shutuma hizi zimekanushwa na Mykhailo Podolyak mshauri wa Ukraine ambaye amesema nchi yake haihusiki na haifahamu lolote kuhusu madai ya serikali ya Urusi.
Taarifa zaidi kutoka Moscow, zinasema ndege hiyo isiyokuwa na rubani ilikuwa imelenga makaazi ya rais maarufu kama Kremlin, lakini rais Putin hakuwepo wakati wa jaribio hilo.
Moscow inasema, kitendo hicho ni cha kigaidi na jaribio la kumuua kiongozi wake wa nchi na ina haki ya kulipiza kisasi.