Pensheni: Maandamano zaidi yashuhudiwa nchini Ufaransa
NAIROBI – Maandamano makubwa yameendelea kushuhudiwa nchini Ufaransa, kuendelea kupinga mageuzi ya rais Emmanuel Macron, kuhusu mfumo wa pensheni nchini humo.
Imechapishwa:
Mwendelezo wa maandamano haya, unakuja baada ya waadamanaji zaidi ya Milioni moja, wiki hii kujitokeza katika miji mbalimbali, kuonesha hasira zao, dhidi ya mageuzi hayo ya rais Macron, ambaye anataka umri wa kuustafu uongezwe kutoka umri wa miaka 62 hadi 64.
Maandamano na migomo ya wiki hii, yalisababisha kukwama kwa huduma za uchukuzi katika miji mbalimbali ikiwepo huduma ya kupata mafuta.
Rais Macron anasisitiza kuwa, kuna umuhimu mkubwa wa kuongeza muda huo wa kustaafu ili kuhakikisha kuwa mfuko wa taifa wa Hifadhi ya Jamii unaimarika zaidi katika miaka ijayo.
Hata hivyo, vyama vya wafanyakazi nchini humo vinaendelea kusisitiza kuondolewa kwa mswada huo wa mageuzi hayo, unaoendelea kujadiliwa na Maseneta, unaotarajiwa kupitishwa kwa sababu Macron ana kura nyingi kwenye Baraza hilo.
Kura za maoni nchini Ufaransa zimeendelea kuonesha kuwa, raia wa nchi hiyo, wanapinga mageuzi hayo, huku wanasiasa wa mrengo wa kushoto wakitaka kampuni na matajiri kulipia zaidi mfuko huo wa pensheni.