Raia wa Ukraine watahadharishwa watarajie mashambulio ya makombora
NAIROBI – Raia wa Ukraine wametahadharishwa na maafisa wa Inteljensia nchini humo kuwa, watarajie mashambulio ya makombora kutoka kwa wanajeshi wa Urusi, hapo kesho, mwaka mmoja kamili tangu Moscow ilipoivamia Ukraine.
Imechapishwa:
Cheza - 00:50
Tahadhari hii inakuja, wakati huu Umoja wa Mataifa, ukitarajiwa kupitisha azimio la kulaani hatua ya Urusi kuivamia Ukraine, na kutoa wito wa amani haraka iwezekanavyo.
Tayari Katibu Mkuu wa Umoja huo Antonio Guteress, amelaani tisho la rais Vladmir Putin kutumia silaha za nyuklia.
Naye rais Volodymyr Zelensky amesema anaamini kuwa nchi yake itashinda vita hivyo, akisema wote walioivamia nchi yake, watawajibishwa.
Wiki hii, rais Putin alitangaza kuendelea kuivamia Ukraine huku akiyashatumu mataifa ya Magharibi yakiongozwa na Marekani, kwa kuchochea vita vinavyoendelea.
Rais wa Marekani Joe Biden, baada ya ziara yake ya kushtukiza jijini Kiev na baadaye kukutana na wakuu wa jeshi la NATO nchini Poland, alisisitiza kuwa, mataifa hayo yataendelea kusimama na kuisaidia Ukraine.