Brazil: Polisi wamefanikiwa kuyadhibiti tena majengo katika mji mkuu Brasilia
Vyombo vya usalama nchini Brazil, vimefanikiwa kuyadhibiti tena majengo ya bunge la kitaifa na yale ya mahakama ya juu, baada ya mamia ya wafuasi wa rais wa zamani, Jair Bolsonaro, kuvamia vyombo hivyo vyenye mamlaka.
Imechapishwa:
Katika tukio ambalo limefananishwa na kilichotokea January 6 mwaka 2021 nchini Marekani, ambapo wafuasi wa Donald Trump walivamia majengo ya bunge, polisi wa Brazil walilazimika kutumia nguvu ikiwemo mabomu ya machozi na risasi za mpira kuwadhibiti wafuasi wa Bolsonaro.
Rais mpya wa Brazil, Lula Inacio da Silva, amekashifu vurugu hizi akiwaita wafuasi wa Bolsonaro, wabaguzi huku akiapa kuwashughulikia kisheria.
Aidha baada ya karibu saa 6 kupita, Bolsonaro ambaye kwa sasa anaishi nchini Marekani, aliandika kupitia ukurasa wake wa kijamii akiwakosoa na kulaani vurugu zilizofanywa.
Katika hatua nyingine viongozi mbalimbali wa dunia akiwemo rais wa Ufaransa na Marekani, wamekashifu kile walichosema jaribio la kubadili maamuzi ya wananchi, wakati huu watu zaidi ya 100 wakikamatwa.