Ufaransa: Walimu na wanafunzi watoa heshima kwa Samuel Paty miaka 2 baada ya kuuawa kwake
Mnamo Oktoba 16, 2020, Samuel Paty, mwalimu wa historia na jiografia, aliuawa katikati ya barabara wakati akitoka chuo chake huko Conflans-Sainte-Honorine, siku kumi baada ya kuonyesha wanafunzi wa darasa lake katuni za Muhammad kutoka gazeti la Charlie Hebdo.
Imechapishwa:
Kuanzia Ijumaa tarehe 14 hadi Jumatatu Oktoba 17, walimu wote wamealikwa na Wizara ya Elimu nchini Ufaransa kutoa heshima kwa mwalimu huyo kulingana na taratibu walizochagua.
Miaka miwili baada ya kuuawa kwa Samuel Paty, walimu na wanafunzi watatoa heshima zao nchini Ufaransa kote kwa mwalimu aliyeuawa katika hali ya wasiwasi kuhusu kuheshimu dini na sheria inayokataza alama za kidini shuleni.
Tukio hilo liliamsha hisia nyingi nchini kote. Kama mnamo Oktoba 2021, shule, vyuo na shule za upili zilialikwa na Wizara ya Elimu kutoa heshima kwa profesa huyo.
Christine Guimonet ni naibu kiongozi wa Chama cha Walimu wa Historia na Jiografia nchini Ufaransa. Anaibua hitaji la dharura la kusaidia walimu katika ufundishaji wao:
"Ni wazi kuna kabla na baada. Ukweli rahisi wa kujua kwamba profesa ameuawa haukubaliki. Ilishangaza sana [...]. Mwalimu anaposhambuliwa na wazazi au wanafunzi, katika kazi yake ya kitaaluma, anapoulizwa, anapokosolewa, ni lazima aweze, bila kuwa na mjadala kuhusiana na suala hilo au mazungumzo, kupokea msaada kutoka kwa wenzake na kisha kuungwa mkono kutoka kwa uongozi katika ngazi zote. Hilo ni la msingi."
Kujenga jamii yenye uvumilivu zaidi
Olivier, profesa wa historia na jiografia katika chuo cha Seine-Saint-Denis, analaani vikali shambulio hilo la kigaidi. Hata hivyo, anaeleza kwamba aliamua kutotoa heshima kwa profesa huyo yeye na wanafunzi wake.