Ukraine: Malengo ya Urusi 'yatatimizwa hata iweje', Putin asema
Rais wa Urusi Vladimir Putin amesisitiza kuwa malengo ya 'operesheni ya kijeshi nchini Ukraine' yatafikiwa.
Imechapishwa:
Kwa mara ya kwanza Ukraine imetangaza juu ya uwezekano wa kuhusika kwake katika miripuko ambayo imekuwa ikitokea katika mikoa ya Urusi iliyo karibu na Ukraine siku za hivi karibuni.
Kwa upande mwingine mikutano na mashauriano vimekuwa vikiendelea katika nchi za Umoja wa Ulaya, baada ya Urusi kuzifungia Poland na Bulgaria mgao wa gesi, kufuatia hatua ya nchi hizo kukataa kulipia huduma hiyo kwa sarafu ya Urusi ya Ruble kama ilivyoamuliwa na rais Vladimir Putin.
Wakati huo huo Halmashauri Kuu ya Umoja wa Ulaya leo imependekeza kuondolewa kwa ushuru kwa forodha kwa bidhaa zote kutoka Ukraine katika hatua ya karibuni kabisa ya kusaidia kuimarisha uchumi wa taifa linalokabiliwa na vita.
Kiongozi wa chombo hicho cha juu ndani ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Layen amesema wamekubaliana na rais Volodymyr Zelensky wa Ukraine kuwa pendekezo hilo ni muhimu katika kuupiga jeki uchumi wa Ukraine unaoyumbayumba.
Pendekezo hilo linataka mataifa ya Umoja wa Ulaya yaruhusu kuingizwa kwa bidhaa zinazozalishwa Ukraine bila kuzitoza ushuru kwa kipindi cha mwaka mmoja.
Hata hivyo bunge la Ulaya na mataifa 27 wanachama wa kanda hiyo watapaswa kwanza kuridhia pendekezo hilo kabla ya kuanza kutekelezwa.