Ukraine: Milipuko huko Transnistria, Moldova yahofia kuongezeka kwa mzozo
Katika siku ya 62 ya uvamizi wa Urusi nchini Ukraine, milipuko mitatu na "shambulio la kigaidi" vimeripotiwa katika eneo linalotaka kujitenga la Moldova la Transnistria na hali hiyo inazua hofu kwamba mzozo wa Ukraine utaenea hadi Moldova.
Imechapishwa:
► Mamlaka inayotaka kujitenga kwa Moldova huko Transnistria imelaani "shambulio la kigaidi" dhidi ya kitengo cha kijeshi Jumanne asubuhi, pamoja na milipuko kwenye mitambo miwili ya redio na Wizara ya Usalama wa Umma Jumatatu jioni. Matukio hayo yanazidisha hofu ya kuongezeka kwa mzozo nchini Moldova, ambayo imeamua kuitisha kwa dharura baraza lake la usalama la kitaifa.
► Mkuu wa Pentagon Lloyd Austin alisema siku ya Jumatatu kuwa Ukraine inaweza kushinda vita hivyo, siku moja baada ya ziara ya kwanza ya viongozi wa Marekani mjini Kyiv tangu uvamizi wa Urusi. "Wanaweza kushinda ikiwa wana vifaa vinavyofaa, usaidizi unaofaa," alisema baada ya kukutana na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky, akiambatana pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje Antony Blinken.
► Uingereza inadai kuwa Urusi inajaribu kuzingira ngime za wanajeshi wa Ukraine mashariki mwa nchi. Kulingana na Wizara ya Ulinzi ya Uingereza, mapigano makali yameripotiwa kusini mwa Izium, huku majeshi ya Urusi yakijaribu kusonga mbele kuelekea miji ya Sloviansk na Kramatorsk kutoka kaskazini na mashariki.
► Idadi ya wakimbizi wanaokimbia uvamizi wa Urusi inazidi milioni 5.2, kulingana na Umoja. Zaidi ya watu milioni 7.7 wametoroka makazi yao lakini bado wako Ukraine.