Urusi yaapa kuishambulia Kyiv kufuatia shambulizi kwenye ardhi yake
Urusi inatishia kutekeleza mashambulizi zaidi jijini Kyiv nchini Ukraine, baada ya kuishtumu nchi hiyo kushambulia miji yake, iliyo mpakani.
Imechapishwa:
Urusi inasema, Ukraine ilituma helikopta mbili za kijeshi kwenda kushambulia mji ulio katika jimbo la Bryansk na kuwajeruhi watu saba akiwemo mtoto mchanga, wakati huu Umoja wa Mataifa ukisema vita hivi vimesababisha watu Milioni tano kukimbia Ukraine.
Hata hivyo, Ukraine imekanusha madai hayo ya Urusi ambayo imeelezea shambulizi hilo kuwa la kigaidi, huku meli yake iliyoshambuliwa ikizama baharini.
Jeshi la Urusi limethibitisha kushambulia kiwanda cha kijeshi nje ya jiji la Kyiv kwa kwa kutumia makombora ya masafa marefu huku Ukraine nayo ikiishtumu Urusi kwa jeshi lake kuwauwa watu saba na kuwajeruhi wengine Mashariki mwa nchi yake wakati, mabasi yakiwasafirisha raia.
Aidha, jeshi la Urusi linasema limewauwa mamluki 30 wa Poland wanaoshirikiana na wanajeshi wa Ukraine katika mji wa Kharkiv.
Wakati hayo yakijiri, Urusi imeonya na kusema itazichukulia hatua nchi za Finland na Sweden iwapo zitajiunga na jeshi la nchi za Magharibi NATO.