Vita nchini Ukraine: Uingereza yachunguza matumizi ya silaha za kemikali
Vikosi vya Urusi siku ya Jumanne vimeendelea kutoa shinikizo lao kwa mji wa kimkakati wa bandari wa Mariupol wakati huko mashariki, Kyiv inatarajia mashambulizi makubwa hivi karibuni.
Imechapishwa:
Kiongozi wa waasi wanaotaka kujitenga wanaounga mkono Urusi mjini Donetsk alisema Jumatatu kwamba vikosi vyake vimeliteka kabisa eneo la bandari la mji wa kimkakati wa Mariupol, kusini mashariki mwa Ukraine, ambalo lilikuwa limezingirwa kwa zaidi ya mwezi mmoja.
Hata hivyo kamanda wa kikosi cha wanajeshi wa Ukraine Valerii Zaluzhnyi alisema kuwa mtandao unaounganisha wanajeshi wanaolinda Mariupol bado haujakatika. Wapiganaji wanaotaka kujitenga wamekuwa wakipigana kwa wiki kadhaa wakiunga mkono jeshi la Urusi kuweza kuudhibiti mji wa kimkakati wa Mariupol.
Wakati huo huo Meya wa mji wa bandari wa Mariupol amesema zaidi ya raia 10,000 wamefarikikatika mzingiro wa Urusi kwenye mji huo, na kwamba idadi ya vifo inaweza kupindukia 20,000 kutokana na miili "iliyotapakaa mitaani"
Kwa hatua nyingine mamlaka nchini Ukraine zimesema huenda maelfu ya watu wameuawa kufuatia mashambulizi ya Urusi katika mji wa bandari wa Mariupol, na kuishtumu Urusi kuchelewesha kimakusudi zoezi la kuhamisha watu kutoka mji huo uliozingirwa, ambao unatajwa kuwa uko katika hali mbaya.