New Caledonia kuendelea kuwa chini ya milki ya Ufaransa
Wakaazi wa visiwa vya New Caledonia vinavyomilikiwa na Ufaransa, wamepiga kura kwa asilimia 96.49 kukataa kujitenga na kuwa taifa huru.
Imechapishwa:
Baada ya uamuzi huo, rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amesema kipindi cha mpito kitaanza kushuhudiwa katika visiwa hivyo, huku akisema Ufaransa inapendeza zaidi ikiwa pamoja na visiwa hivyo vyenye watu zaidi ya Laki Mbili na Elfu Sabini.
Aidha, kiongozi huyo wa Ufaransa amesema, baada ya kura hiyo ya maoni na wakaazi wa visiwa hivyo kuamua kusalia kama sehemu ya Ufaransa, sasa wakati umefika wa kujenga umoja thabiti.
Matokeo yanaonesha kuwa, ni asilimia 3.51 ya wapiga kura ndio waliounga mkono kwa visiwa hivyo vinavyopatikana Kusini mwa Bahari ya Pacif kujitenga na Ufaransa na kuunda taifa lao.
Hata hivyo ni asilimia 43.90 ya wapiga kura, ndio walioshiriki kwenye zoezi la kura hiyo ya maoni huku wanaharakati waliokuwa wanataka visiwa hivyo kujitenga, wakisusia kura hiyo baada ya kutaka ifanyike mwezi Septemba mwalka ujao ili kuwaruhusu kuwa na muda wa kutosha kufanya kampeni.