Zaidi ya kesi mpya 6,400 zathibitishwa nchini Ujerumani
Idadi ya visa vya maambukizi ya virusi vya Corona vilivyothibitishwa nchini Ujerumani imepanda hadi 2,148,077, baada ya visa 6,408 kuthibitishwa siku moja iliyopita, kulingana na takwimu zilizotolewa leo Taasisi ya kuzuia na kudhibiti magonjwa ya kuambukia ya Robert Koch (RKI).
Imechapishwa:
Taasisi hiyo pia inaripoti vifo vipya 903, na kufikisha jumla ya vifo 52,990 tangu kuzuka kwa janga hilo nchini Ujerumani.
Jumatatu wiki hii serikali ya Ujerumani ilisema kuwa ina wasiwasi kuhusu maambukizi ya aina mpya ya kirusi cha Corona kilichogundulika kwa mara ya kwanza Uingereza.
Msemaji wa serikali Steffen Seibert alisema kirusi hicho kinaweka hatari kubwa nchini, ambapo mpaka sasa kuna idadi ndogo ya visa vilivyogundulika. Amesema maambukizi ya virusi vya corona yameanza kupungua kutokana na hatua zilizowekwa na serikali.
Hayo yanajiri wakati Halmashauri Kuu ya Ulaya imependekeza kuwa mataifa yote ya Umoja wa Ulaya yaimarishe mipaka yao, na kuwataka wasafiri kutoka nchi zisizo mwanachama wa umoja huo kuwasilisha vipimo vyao vya kuonyesha kuwa hawana maambukizi ya virusi vya Corona ambavyo vina chini ya saa 72 kabla ya kuanza safari yao.
Kamishna wa Sheria wa Umoja wa Ulaya Didier Reynders alisema kuwa ipo haja ya dharura ya kupunguza kitisho cha maambukizi kinachohusiana na usafiri ili kupunguza mzigo wa mifumo ya afya iliyoelemewa. Alibaini kwamba kuna viwango vikubwa vya maambukizi katika mataifa mengi wanachama.