Coronavirus: Zaidi ya kesi mpya 6,800 za maambukizi zathibitishwa Ujerumani
Idadi ya kesi zilizothibitishwa za maambukizi ya virusi vya Corona nchini Ujerumani imepanda hadi 373,167, baada ya visa zaidi ya 6,868 kuthibitishwa siku moja iliyopita, kulingana na takwimu zilizotolewa leo Jumanne na kituo cha kuzuia na kudhibiti magonjwa cha Robert Koch (RKI).
Imechapishwa:
Kituo cha kuzuia na kudhibiti magonjwa cha Robert Koch (RKI) kimerekodi vifo zaidi ya arobaini na saba na kufanya jumla ya vifo kufikia 9,836 tangu kuzuka kwa janga hilo nchini.
Ongezeko la kimataifa la maambukizi la wiki za hivi karibuni limekuwa likishuhudiwa zaidi barani Ulaya, ambako zaidi ya watu 240,000 wamefariki kutokana na janga hilo hadi sasa.
Idadi ya maambukizi ya virusi vya Corona imepindukia milioni 40 kote ulimwenguni. Kulingana na Chuo Kikuu cha John Hopkins ambacho kinakusanya takwimu kutoka kote duniani, idadi hiyo ilipindukia hapo jana. Aidha wataalamu wamesema idadi halisi inaweza kuwa kubwa zaidi ya hiyo.
Hadi sasa, zaidi ya watu milioni 1.1 wamefariki kutokana na virusi vya Corona, ingawa wataalamu pia wanaamini idadi halisi inaweza kuwa kubwa zaidi ya hiyo. Marekani, India na Brazil ndiyo mataifa yanayoripotiwa kuwa na idadi kubwa zaidi ulimwenguni kote.