Serikali ya Ujerumani yapiga marufuku kundi la Hezbollah katika ardhi yake
Ujerumani imetangaza kundi la Hezbollah kutoka Lebanon kuwa ni kundi la kigaidi na imepiga marufuku vuguvugu hilo la Kishia linaloungwa mkono na Iran kuendesha harakati zake nchini humo, Waziri wa Mambo ya Ndani, Horst Seehofer amesema.
Imechapishwa:
Waziri Horst Seehofer amebaini kwamba operesheni kabambe imefanyika mapema Alfajiri leo Alhamis ili kuwakamata wanamgambo wa kundi hilo.
Wawakilishi wa idara za usalama nchini Ujerumani wanabaini kwamba karibu watu elfu moja nchini Ujerumani wana uhusiano na kundi la Hezbollah.
"Waziri wa Mambo ya Ndani Horst Seehofer amepiga marufuku kundi la kigaidi la Kishia la Hezbollah nchini Ujerumani," msemaji wa wizara ya mambo ya ndani ameandika kwenye Twitter.
Kufikia sasa, Berlin imekuwa ikitofautisha kati ya tawi la kisiasa la Hezbollah na vitengo vyake vya jeshi, ambavyo vimepigana nchini Syria vikisaidia vikosi vya serikali ya Bashar al Assad.