Obama atangaza nchi yake kutoa msaada wa dola bilioni 1 kwaajili ya Usalama kwenye ukanda wa Ulaya
Rais wa Marekani Barack Obama siku ya Jumanne ametangaza mpango wa nchi yake kutoa kiasi cha dola bilioni 1 kwaajili ya kusaidia kuimarisha usalama kwenye eneo la mashariki mwa Ulaya.
Imechapishwa:
Rais Obama ametoa ahadi hiyo alipkuwa mjini Warsaw nchini Poland, ambapo amemuhakikishia rais wa taifa hilo kuwa nchi yake itahakikisha kiasi hichi cha fedha kinapatikana kusaidia kuimarisha usalama kwenye eneo la Ulaya.
Kauli ya rais Obama anaitoa wakati huu kukiwa na wasiwasi wa kuzuka kwa vita baridi kati ya mataifa ya Ulaya na nchi ya Urusi inayotuhumiwa na mataifa haya ya Ulaya kufanya uvamizi kwenye taifa la Ukraine.
Rais Obama juma hili alitangaza kufanya ziara kubwa kwenye nchi za Ulaya ambapo pia atahudhuria sherehe za miaka 25 ya nchi ya Poland toka kufanyika kwa uchaguzi wa kwanza wa kidemokrasia.
Sherehe za mwaka huu zinafanyika wakati ambapo nchi za mashariki mwa Ulaya zimeingiwa na hofu kufuatia hatua za hivi karibuni za nchi ya Urusi kuonekana kana kwamba inataka kurejesha kwa nguvu nchi zilizokuwa zimejitenga na Urusi wa kati wa utawala wa kisoviet.
Kwenye mkutano wake na wanahabari, rais Obama amesema kuwa atawasilisha ombo maalumu kwenye bunge la Congress kuomba idhini kwa wabunge wake kupitisha kiasi cha dola bilioni 1 fedha zitakazotumika kuimarisha usalama kwenye nchi za mashariki mwa Ulaya.
Rais Obama anasema kuwa "Utayari wetu kuisaidia nchi ya Poland kiusalama pamoja na washirika wetu wa mashariki na kati ya Ulaya ni jambo la msingi na tunalipa kipaumbele." Obama alisema.
Kwa upande wake rais wa Poland, Bronislaw Komorowski amesisitiza kutotambua kile kilichofanywa na nchi ya Urusi kwenye taifa la Ukraine kwa kulichukua kwa nguvu eneo la Crimea ambalo lilikuwa ni eneo halali la nchi ya Ukraine.