Mladic aswekwa jela, huko The Hague, baada ya kutolewa Serbia
Mtuhumiwa wa mauaji ya halaiki nchini Bosnia Ratko Mladic amewekwa jela katika mahakama ya makosa ya kivita ya Umoja wa Mataifa jana jioni, huko The Hague Uholanzi.Hatua hiyo inakuja baada ya ombi lake la kutotolewa nchini Serbia, kugonga mwamba.
Imechapishwa:
Kwa mujibu wa maelezo ya msemaji wa mahakama hiyo Nerma Jelacic, madaktari walianza na kuchukua vipimo vya afya ya Mladic katika mahakama hiyo, inayowashikilia watuhumiwa wa mahakama ya kimataifa ya uhalifu katika Yugoslavia ya zamani.
Kabla ya kukutana ana kwa ana na hakimu, Jelacic anapasha kuwa mtuhumiwa huyo aliyekuwa mafichoni kwa takriban miaka kumi na sita, atatengwa sehemu ya peke yake kwa saa 48, mfululizo.
Akithibitisha taarifa hiyo, balozi wa Bosnia nchini Uholanzi anasema muda huo ni mrefu sana kwa jenerali huyo wa zamani, aliyekuwa akiongea sana alipofika nchini Uholanzi.
Mladic alikuwa kamanda wa majeshi ya Bosnia na Serbia wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe, nchini Bosnia-Herzegovina, machafuko yaliyosababisha wengi kumwaga damu zao na hatimaye kulivunja taifa la Yugoslavia.
Anakabiliwa na tuhuma za mauaji ya halaiki, uhalifu dhidi ya binadamu na ukiukaji wa haki za kivita. Alikamatwa siku ya Alhamis, iliyopita.