Baraza la usalama la UN kukutana wiki ijayo baada ya uamuzi wa ICJ
Nairobi – Baraza la usalama katika Umoja wa Mataifa litakutana wiki ijayo baada ya uamuzi wa mahakama ya juu zaidi duniani inayoitaka Israel kuzuia vitendo vya mauaji ya halaiki huko Gaza, ofisi ya rais wa baraza hilo imethibitisha.
Imechapishwa:
Mkutano huo wa Jumatano uliitishwa na Algeria, ambayo wizara yake ya mambo ya nje ilisema unatarajia kujadili na kuangazia umauzi uliotolewa na mahakama hiyo dhidi ya Israel.
Mahakama ya ICJ siku ya Ijumaa ilisema Israel lazima izuie vitendo vya mauaji ya halaiki katika vita vyake na Hamas na kuruhusu misaada kuingia Gaza, bila ya kutoa agizo la kusitishwa kwa mapigano.
Baraza la Usalama, ambalo limegawanyika kwa muda mrefu kuhusu suala la Israel na Palestina, limekubali maazimio mawili pekee tangu mashambulio ya Oktoba 7 ya Hamas dhidi ya Israel.
Mapigano ya sasa yalianza baada ya Hamas kutekeleza shambulio dhidi ya Israel ambalo lilisababisha vifo vya takriban watu 1,140 nchini Israeli kwa mujibu wa takwimu za mamlaka nchini humo.
Wapiganaji wa Hamas pia waliwateka watu 250 na Israel inasema karibu 132 kati yao bado wanazuiliwa huko Gaza, ikiwa ni pamoja na miili ya mateka 28 waliokufa.
Israel imeapa kuwaangamiza Hamas ambapo imeanzisha mashambulio ya kijeshi ambayo wizara ya afya huko Gaza inasema yameua takriban watu 26,083, takriban asilimia 70 kati yao wanawake na watoto.