Israel kuendelea na vita dhidi ya Hamas mwaka wote wa 2024
Nairobi – Israel imeonya kuwa vita vyake dhidi ya kundi la Hamas vitaendelea mwaka huu wote wa 2024.
Imechapishwa:
Msemaji wa jeshi la ulinzi la Israel Daniel Hagari katika ujumbe wake wa mwaka mpya, ameeleza kuwa karibia wanajeshi laki tatu wa akiba watapumzishwa kutoka kwenye mapigano ilikujiandaa kwa mapambano ya muda mrefu na kujipanga upya.
Hadi sasa, zaidi ya watu 21,800 wameuawa huko Gaza, wengi wao wakiwa watoto na wanawake, kulingana na wizara ya afya inayoendeshwa na Hamas.
Haya yanajiri wakati huu makabiliano kati ya Israel na Hamas yakiingia katika wiki ya kumi na moja sasa.
Makabiliano yalianza tarehe 7 Oktoba mwaka wa 2023 baada ya wapiganaji wa Hamas kuvuka mpaka na kutekeleza shambulio ambalo halijawahi kushuhudiwa kusini mwa Israel.
Shambulio hilo la Hamas lilisababisha vifo vya watu 1,200, wengi wao wakiwa raia na wengine wapatao 240 walichukuliwa mateka.
Israel imeahidi kumaliza wapiganji wa Hamas, jeshi likisema kuwa maofisa wake 172 wameuawa katika ukanda wa Gaza wakati wa vita dhidi ya kundi hilo ambalo Israeli, Marekani na Umoja wa Ulaya zinasema ni la kigaidi.
Siku ya Jumamosi, waziri mkuu wa Israeli, Benjamin Netanyahu alionya kuwa vita vitaendelea kwa muda wa miezi kadhaa hadi pale ambapo kundi la Hamas litaisha na kurejeshwa kwa mateka wote.