Israeli imekubali kusitisha mashambulio dhidi ya Gaza kuruhusu raia kuondoka
Nairobi – Israeli imekubali wito wa kusitisha mashambulio yake kaskazini mwa Gaza ilikuruhusu baadhi ya raia kuondoka katika maeneo yanayoshudia mapigano mazito.
Imechapishwa:
Licha ya kutangaza hatua hiyo, waziri mkuu Benjamin Netanyahu amesema hatua yoyote ya kusitisha mapigano haimaanishi wamejisalimisha kwa Hamas.
Rais wa Marekani Joe Biden ambaye nchi yake ni mojawapo ya mataifa ambayo yamekuwa yakiongoza wito wa kusitishwa kwa mapigano amekaribisha hatua hiyo ya Israeli.
Tayari maelfu ya raia wa Palestina wametoroka kaskazini mwa Gaza kwa kuhofia kushambuliwa katika makabiliano yanayoendelea.
Netanyahu aidha, amewapongeza wanajeshi wa nchi yake katika vita dhidi ya Hamas ambao walitekeleza shambulio mbaya zaidi katika historia ya Israeli mwezi Oktoba tarehe saba.
Raia 1,400 wa Israeli waliripotiwa kufariki katika shambulio hilo la Hamas wakati wengine karibia 240 wakitekwa.
Kwa upande mwengine, wizara ya afya katika ukanda wa Gaza inayoongozwa na Hamas imesema raia wa Palestina zaidi ya 10,800 wakiwemo watoto na wanawake, wameuawa katika mashambulio ya Israeli.
Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshugulikia wahamiaji nchini Palestine UNRWA, limesema watu elfu 70 wametoroka kusini mwa Gaza tangu tarehe 4 ya mwezi Novemba, wengi wao wakitembea kwa miguu.
Karibia watu 1.6 wamepoteza makazi yao tangu tarehe 7 ya mwezi Oktoba katika eneo la Gaza.