Watu 25 wauawa huku wasiwasi ukiongezeka kati ya Israeli na Palestina
NAIROBI – Mapigano kati ya Israeli na Gaza yameendelea kushuhudiwa mapema Alhamisi, hii ikiwa ni siku ya tatu ya ongezeko la ghasia tangu katikati ya mwaka jana katika eneo la pwani ya Palestina.
Imechapishwa:
Maofisa wa Gaza wamesema mashambulizi ya anga na makombora kutoka Israel, yamewauwa Wapalestina 25 tangu Jumanne miongoni mwao wapiganaji na raia.
Mapema Alhamisi, maduka katika Gaza yalifungwa huku barabara zikiachwa pweke kwa kiasi kikubwa wakati ndege za kijeshi za Israel zikizunguka eneo hilo ambapo majengo kadhaa yalikuwa magofu.
Zaidi ya maroketi 500 yalirushwa kutoka Gaza tangu Jumanne, jeshi likisema hakuna maafa yaliyoripotiwa.
Kundi la Islamic Jihad limethibitisha kupoteza viongozi wake wanne katika mashambulio haya, wa hivi punde akiwa Ali Ghali, kamanda wa kitengo cha kurusha roketi.
Kundi jingine la Popular Front for the Liberation of Palestine, pia lilisema wapiganaji wake wanne wameuawa.
Jumatano Mei 10, waziri mkuu wa Israeli Benjamin Netanyahu kwenye hotuba yake kupitia runinga, alisema kuwa wataendelea kukabiliana na waasi.
Tunawaambia magaidi na wale wanaowatuma: tunawaona kila mahali, humuwezi kujificha, na tunachagua mahali na wakati wa kukupiga.
Mapigano mabaya
Mapigano ya wiki hii ya Gaza ni mabaya zaidi tangu yale ya mwezi Agosti ambayo yaliwauwa Wapalestina 49, mzozo ambao umekuwa ukiongezeka tangu kiongozi Netanyahu aliporejea madarakani mwishoni mwa mwaka jana akiongoza muungano wenye vyama vya mrengo wa kulia na vya Orthodox.
Nchi ya Marekani na Israeli zinayachukulia makundi ya Hamas, na Islamic Jihad, kuwa makundi ya kigaidi.
Ghasia pia zimepamba moto katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu, ambapo jeshi la Israel limekuwa likifanya mashambulizi ya mara kwa mara dhidi ya wanamgambo.