Iran: Kituo cha nyuklia cha Natanz chahujumiwa na kitendo cha "ugaidi"
Kituo cha nyuklia cha Natanz Kusini kwa mji wa Tehran nchini Iran, kimeshuhudia hitilafu siku moja, baada ya kuzinduliwa kwa mtambo wake wa kurutubisha madini ya Uranium.
Imechapishwa:
Mkuu wa mradi wa nyuklia nchini humo Ali Akbar Salehi amesema hitilafu iliyoshuhudiwa katika kituo hicho na kusababisha kupotea kwa nguvu za umeme ni kitendo cha kigaidi.
Hata hivyo, Salehi haikutaja ni nani aliyehusika lakini ripoti kutoka Israel, zinasema kuwa, kituo hicho kilishambuliwa na Israel, lakini nchi hiyo haijasema lolote.
Hata hivyo, hivi karibuni Israel imekuwa ikionya, kuhusu mradi wa nyuklia wa Iran na kusema unahatarisha usalama wake.
Iran sasa inataka Jumuiya ya Kimataifa kulaani kitendo hicho, huku ikisema inaendelea na uchunguzi kubaini ukweli wa kilichotokea.
Shambulio hilo limekuja siku chache tu baada ya Iran kuanza mazungumzo ya kuishawishi Marekani kurejea tena kwenye mkataba wa nyuklia uliotiwa saini mwaka 2015 kati yake na nchi za Magharibi.