Uturuki yaendelea na mashambulizi dhidi ya wapiganaji wa Kikurdi Syria
Uturuki imeendeleza mashambulizi dhidi ya wapiganaji wa Kikurdi nchini Syria. Huku umoja wa mataifa ukisema una wasiwasi na hali ya kibinadamu katika eneo la Afrin.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Rais Recep Tayyip Erdogan amesema mashambulizi haya yataendelea hadi pale, wapiganaji hao watakapoondolewa katika jimbo la Afrin.
Hata hivyo Marekani ambayo inawaunga mkono wapiganaji hawa, imeitaka Uturuki kuwa makini katika mashambulizi yake ili kuepuka kuuawa kwa raia.
Uturuki inasema, wapiganaji wa Kikurdi ni magaidi.
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ambalo lilikutana jana Jumatatu (Januari 22) kujadili hali ya kibinadamu kaskazini mwa Syria, halikulaani au kushtumu Uturuki kuingia kijeshi nchini Syria. Ufaransa ilikuwa imeomba kuepo na mkutano wa dharura kuhusu mashambulizi ya Uturuki katika eneo la Afrin.
Hata hivyo wajumbe wa Baraza la Usaam ala Umoja wa Mataifa walionesha wasiwasi wao kuhusu hali ya kibinadamu kufuatia mashambulizi ya Uturuki katika eneo hilo la Afrin, ambapo hakuna msaada wowote ambao umewafikia walengwa katika mji wa Idleb tangu mwezi Novemba.