Watu zaidi ya 35 wauwawa nchini Iraq kufuatia mashambulizi ya mabomu
Watu zaidi ya thelathini na watano wameuawa huku wengine zaidi ya mia moja wakijeruhiwa kufuatia mfululizo wa mashambulizi ya mabomu yaliyowalenga watu wa jamii ya kishia katika mji mkuu wa Iraq, Baghdad.
Imechapishwa:
Polisi wamesema mashambulizi ya mabomu kumi na moja yalitekelezwa katika ghasia za siku ya Jumatano kwenye miji ya Baghdad, Kirkuk, Mosul na Tarmiyah.
Mashambulizi hayo yamekuja siku moja tu baada ya watu wengine kumi na sita kuuawa na wanamgambo waliovamia maduka ya pombe kali mjini Baghdad.
Hali ya wasiwasi imekuwa ikiongezeka miongoni mwa jamii za madhehebu ya washia na wasuni huku lawama zikizidi kuelekezwa kwa serikali ya waziri Mkuu Nuri al-Malik kwa kushindwa kukomesha ugaidi unaofadhiliwa na mtandao wa kigaidi duniani wa Al-Qaeda katika nchi hiyo.