Malawi kupeleka mzozo wa mpaka kati yake na Tanzania katika Mahakama ya Kimataifa
Malawi inasema itawasilisha mgogoro kuhusu mpaka wa Ziwa Nyasi kati yake na Tanzania katika Mahakama ya Kimataifa inayoshughulika na maswala ya Mipaka ICJ, baada ya mataifa hayo mawili kushindwa kupata mwafaka.
Imechapishwa:
Rais Joyce Banda amesema kuwa serikali yake imefikia hatua hiyo baada ya kubainika kuwa suluhu kati ya mataifa hayo mawili huenda lisipatikane baada ya Tanzania kutoa ramani nyingine tofauti kuonesha mipaka ya Ziwa hilo,ramani inayopingwa na Malawi.
Hatua ya Tanzania kutoa ramani hiyo mpya ilisababisha Malawi kujiondoa katika mazungumzo ya kupata suluhu mwezi uliopita na hivyo, baada ya kuhisi kuwa suluhu linaweza tu kupatikana katika Mahakama ya ICJ.
Mzozo wa mpaka katiKa Ziwa Nyasa ulizuka baada ya serikali ya Malawi kutoa kibali kwa wataalam kutoka nchini Uingereza kufanya utafiti wa mafuta katika Ziwa hilo karibu na mpaka wa Tanzania.
Mwezi uliopita mazungumzo kati ya serikali ya Lilongwe na Dar es salaam yalivunjika baada ya suluhu kutopatikana kutokana na pande mbili kushikilia msimamo wake.