Kivu Kaskazini: Zaidi ya kaya 700 kutoka Bunagana zafurushwa Uganda
Zaidi ya kaya 700 za Wakongo waliokimbia makazi yao wamefukuzwa tangu Alhamisi, Septemba 1, nchini Uganda.
Imechapishwa:
Kulingana na vyanzo vya utawala, familia hizi zilikuwa zimekimbilia Uganda kupata hifadhi kutokana na mapigano kati ya FARDC na waasi wa M23 katika eneo la Rutshuru katika mkoa wa Kivu Kaskazini.
Vyanzo hivyo vinabaini kwamba takriban familia 400 za watu hawa waliolazimika kuyahama makazi yao ziliwasili Ijumaa, Septemba 2 katika eneo la Rushuru huku wengine zaidi ya 350 wakiwa katika eneo la Busanza.
Wakongo hawa waliolazimishwa kurudi kutoka Kisoro (Uganda), wanapitia kituo kidogo cha mpaka wa Kitagoma na kupokelewa katika eneo la Busanza.
Hatu hii imechukuliwa ili kuepuka kupitia eneo la Jomba linalokaliwa na waasi wa M23, kulingana na Radio Okapi nchini DRC.
Operesheni hizi za kulazimishwa za kuwarudisha nyuma zinafanywa kwa uamuzi wa mamlaka ya Uganda, kulingana na vyanzo kutoka Rutshuru.
Vikosi vya usalama vya Uganda vinawalazimisha Wakongo waliokimbia makazi yao, wanaoishi katika nyumba za kupangisha au katika maeneo ya muda huko Kisoro, ama kupanda mabasi ili kuhamishwa hadi kambi ya wakimbizi ya Nyakabande, kilomita 17 kutoka mpakani, au kwenda katika eneo ambalo bado linakaliwa na M23.
Kwa upande wake, Mkuu wa Eneo la Jomba, Jackson Gachuki, ameomba serikali ya Kongo kuingilia kati ili kulinda haki za Wakongo hao ambao wamepata hifadhi katika nchi jirani ya Uganda.