Baada ya maandamano na umwagaji damu nchini Libya, wanajeshi zaidi wapelekwa mjini Tripoli ili kuimarisha usalama
Wanajeshi wamepelekwa katika mji mkuu wa Libya, Tripoli kufuatia maandamano ya mwishoni mwa juma yaliyofuatiwa na makabiliano yaliyosababisha vifo vya watu zaidi ya 40, ikiwa ni machafuko makubwa kuwahi kutokea tangu mapinduzi ya umma dhidi ya utawala wa marehemu Kanali Muammar Gaddafi mwaka 2011. Taarifa ya serikali ya nchi hiyo imesema wanajeshi wa Taifa wataendelea kuingia katika mji huo wakitokea maeneo mbalimbali ili kuimarisha usalama.
Imechapishwa:
Serikali ya Marekani nayo imeahidi kutoa mafunzo kwa wanajeshi wa Libya ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ulinzi wa Usalama, katika mpango huo wanajeshi wa Libya kati ya 5,000 hadi 8,000 watapatiwa mafunzo.
Hofu ya usalama imeendelea kutanda nchini humo, mwezi oktoba Waziri Mkuu Ali Zeidan naye alitekwa na siku chache baadaye kiongozi wa Ulinzi alikiri kuhusika na utekaji huo.
Mwishoni mwa juma lililopita, Naibu Mkuu wa Usalama wa wa Taifa, Mustafa Nuh aliyetekwa na watu waliojihami kwa silaha jumapili na kuachiwa jana jumatatu.
Baadhi ya raia wamekuwa wakiishutumu serikali kwa kushindwa kudhibiti makundi ya wanamgambo ambao walisaidia kumpindua marehemu Kanali Muammer Ghaddafi.
Katika mkutano wa Mawaziri wa kigeni wa nchi wanachama wa Umoja wa Ulaya EU, walielezea kusikitishwa na hali ya siasa na usalama nchini Libya na kulaani ghasia za Novemba 15 zilizosababisha maafa makubwa.