Wanamgambo 37 wa Boko Haram wauawa Nigeria
Jeshi la nchini Nigeria limesema limewauwa watu thelathini na saba wanaodhaniwa kuwa wanachama wa kundi la wanamgambo wa Boko Haram katika oparesheni iliyoendeshwa jimboni la Borno kaskazini mashariki mwa nchi hiyo.
Imechapishwa:
Msemaji wa jeshi Aliyu Danja amesema walivamia eneo linalodhaniwa kuwa kambi ya wanamgambo hao na kuanzisha oparesheni hiyo iliyofanikiwa pia kuteketezwa kwa mali kadhaa za wapiganaji hao yakiwemo magari na silaha.
Oparesheni hiyo imekuja baada ya mwishoni mwa juma lililopita Boko Haram kuwauwa watu kumi na tisa katika kituo cha ukaguzi wa magari mpakani mwa Nigeria na Cameroon.
Licha ya kutangazwa kwa hali ya hatari na kuundwa kwa vikundi vya ulinzi ili kulitokomeza kundi hilo, bado usalama umeendelea kuwa hafifu katika eneo la kaskazini mwa Nigeria, na tayari watu zaidi ya 3600 wamepoteza maisha yao tangu kuanza kwa harakati za Boko Haram miaka minne iliyopita.
Wanamgambo wa Boko Haram wamekuwa wakifanya harakati zao za mashambulizi wakidai kuundwa kwa taifa la kiislamu sambamba na matumizi ya sharia.