Wanajeshi wa Misri wazingira msikiti wa Al- Fath baada ya waandamanaji kupanga maandamano mapya.
Wanajeshi wa Misri leo Jumamosi wameingia ndani ya msikiti wa Al-Fath jijini Cairo ambako waandamanaji wa kiislamu wamejikusanya kwa usiku mzima siku moja baada ya mapigano ya umwagaji damu kushuhudiwa nchini humo
Imechapishwa:
Picha za moja kwa moja za kituo binafsi cha televisheni nchini humo ONTV zimewaonesha wanajeshi hao wakifanya majadiliano na waandamanaji kujaribu kuwashawishi kuondoka msikitini hapo.
Mmoja wa waandamanaji aliyekuwa ndani ya msikiti huo ameliambia shirika la habari la Ufaransa kuwa wamewataka kutowakamata na kuacha washambuliwe na raia wenye hasira waliopo nje ya msikiti huo.
Vikosi vya usalama nchini Misri mapema hii leo vimeuzunguka msikiti wa Al- Fath uliofurika wafuasi wa kiongozi aliyeondolewa madarakani na jeshi Mohammed Morsi wafuasi ambao wamepanga maandamano mapya baada ya mapigano yaliyosababisha vifo vya watu zaidi ya themanini.
Machafuko hayo yamewagawa wamisri kinyume na ambavyo imewahi kutokea katika historia ya taifa hilo hivi karibuni,wakitofautiana na serikali iliyowekwa madarakani na jeshi pamoja na ushawishi wa mataifa ya kigeni