Mapigano mapya yazuka Syria wakati upinzani ukikutana Qatar katika mazungumzo ya kutafuta suluhu
Waasi nchini Syria wamepambana na Vikosi vya Utawala wa nchini humo mjini Damascus na Aleppo wakati huu ambapo Upinzani ukiwa Nchini Qatar katika Mazungumzo na jitihada za kidiplomasia kumaliza Machafuko nchini Syria.
Imechapishwa:
Mapigano haya mapya yamekuja wakati huu ambapo Waasi wakiendeleza Operesheni zao dhidi ya Serikali baada ya kudhibiti eneo linalozalisha mafuta na kushambulia ndege ya kivita Mashariki mwa Mji wa Deir Ezzor hapo jumapili.
Wakati hayo yakijiri waasi nchini Syria wamegawanyika kuhusu suala la Muungano baina yao, wakati huu ambapo Baraza la Mapinduzi nchini humo likitakiwa kujumuisha waasi wengine walio katika harakati za kuung'oa utawala wa Syria.
Wachambuzi wa masuala ya siasa wanaona kuwa hatua ya kuwepo kwa makundi na hali ya kutoelewana miongoni mwa waasi wanaopambana na vikosi vya rais Bashar Al Assad inachangiwa na baadhi ya makundi ya waasi kuwa na uhusiano na kundi la kigaidi la Al-Qaeda.
Zaidi ya watu 36,000 wamepoteza maisha kufuatia machafuko nchini Syria toka mwezi machi mwaka jana huku juhudi mbalimbali za kutatua mgogoro huo zikionekana kutozaa matunda mpaka sasa.