Matumaini ya kuwapata manusura wa ajali ya meli Zanzibar yadidimia
Matumaini ya kuwapata zaidi ya watu 100 wakiwa hai baada ya meli iliyokuwa na zaidi ya abiria 200 kuzama barani Hindi siku ya Jumatano ikitokea Dar es salaam kwenda visiwani Zanzibar nchini Tanzania yamedidimia.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Maafisa wa uokoaji wanasema matumaini yalididimia baada ya meli hiyo kuzama zaidi ndani ya maji kwa mujibu wa msemaji wa jeshi la polisi kisiwani Zanzibar Mohamed Mhina.
Tayari miili zaidi ya sitini imepatikana na zaidi ya watu wengine zaidi ya mia moja wameokolewa wakiwa hai na wanapata matibabu katika hospitali mbalimbali kisiwani humo.
Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Jakaya Kikwete amesema amesikitishwa mno na ajali hiyo na kutuma risala za rambirambi kwa jamaa ndugu na marafiki wa waathiriwa wa mkasa huo.
Rais wa Zanzibar,Ali Mohammed Shein ametangaza siku tatu za maombolezo kutokana na mkasa huo wa ajali ya meli na kuwakumbuka wale wote waliopoteza maisha yao.
Mwezi Septemba mwaka uliopita,meli nyingine ya abiria ilizama katika bahari Hindi ikitokea Dar es salaam na kusababisha vifo vya mamia ya watu.
Tanzania imekuwa ikikumbwa na visa vya ajali za meli jambo ambalo linazua maswali mengi kuhusu usalama wa safari za majini katika taifa hilo.