Pata taarifa kuu
SYRIA

Watu 20 wapoteza maisha Nchini Syria katika Jiji la Idlib baada ya kutokea kwa mashambulizi

Watu zaidi ya ishirini wamepoteza maisha nchini Syria baada ya kutekelezwa kwa shambulizi lililolenga Majengo ya Ulinzi katika Jiji la Idlib uliopo Kaskazini Magharibi mwa nchi hiyo Tume ya Kutetea Haki za Binadamu ya Syria imethibitisha hilo. Mkuu wa Shirika la Kutetea Haki za Binadamu Nchini Syria Rami Abdel Rahman amesema mashambulizi hayo yalilenga Makao Makuu ya Ofisi za Ulinzi pamoja na nyumba moja ya inayotumiwa na wanajeshi wa anga wa intelijensia.

Mashambulizi ya mabomu yaliyotekelezwa nchini Syria katika Jiji la Idlib na kusababisha vifo vya watu 20
Mashambulizi ya mabomu yaliyotekelezwa nchini Syria katika Jiji la Idlib na kusababisha vifo vya watu 20
Matangazo ya kibiashara

Televisheni ya Taifa ya Syria imesema watu ambao wamepoteza maisha kwenye mashambulizi hayo ni wanane wakiwemo raia huku wengine wakijeruhiwa katika mashambulizi hayo mawili yaliyofanyika huko Idlib.

Taarifa hizo ya Televisheni ya Taifa imesema shambulizi hilo ni la kigaidi na umekuwa muendelezo wa matukio ambayo yamekuwa yanapangwa na wapinzani ili kukwamisha mapendekezo ya Kofi Annan kumaliza umwagaji damu.

Mashambulizi haya yanakuja wakati huu Mkuu wa Waangalizi wa Umoja wa Mataifa UN Meja Jenerali Robert Mood waliopo nchini Syria kufanya tathmini ya utekelezaji wa mapendekezo sita ya Mpatanishi wa Kimataifa wa Mgogoro wa nchi hiyo Koffi Annan ametoa onyo kikosi chake hakina uwezo wa kumaliza machafuko yanayoendelea.

Meja Jenerali Mood amesema waangalizi ambao wapo nchini Syria hawana uwezo wa kumaliza au kukabiliana na machafuko yanayochangia umwagikaji wa damu katika nchi hiyo kwa kuwa hawana silaha na hivyo kazi yao ni kufanya tathmini pekee na si kulinda raia wa nchi hiyo.

Mkuu huyo wa Waangalizi wa Umoja wa Mataifa UN amesema ili kuweza kutekeleza mapendekezo sita ambayo yalitolewa na Mjumbe wa UN na Jumuiya ya Nchi za Kiarabu Annan ili kumaliza umwagaji wa damu ni lazima pande zote zisitishe mapigano kinyume na hapo hawawezi kufanikiwa.

Meja Jenerali Mood ametoa kalipio kwa wale wote ambao wanaendelea kuijaribu serikali ya Rais Bashar Al Assad na kusema hali hiyo itachangia kuibuka kwa mapigano makali zaidi na hivyo kazi ya Annan kwenye usuluhishi wa mgogoro huo itazidi kuwa ngumu na huenda isifanikiwe kabisa.

Timu ya Waangalizi ya Umoja wa Mataifa UN tangu imewasili nchini Syria majuma mawili yaliyopita wamefanikiwa kupunguza kwa kiasi mashambulizi ambayo yamekuwa yakifanyika kati ya Majeshi ya Serikali dhidi ya Wapinzani ambao wanashinikiza mabadiliko ya utawala nchini humo kwa miezi zaidi ya kumi na tatu.

Meja Jenerali Mood ameweka bayana nia yao ni kuhakikisha mapendekezo sita ya Annan yanatekelezwa kwa wakati na wao wapo kusimamia ili lengo liweze kutimia na hatimaye umwagaji wa damu ambao umeshuhudia kwa zaidi ya mwaka mmoja unafikia kikomo ili hali irejee kama awali.

Naye Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Msalaba Mwekundu ICRC Jakob Kellenberger amesema mapendekeo sita ya Annan katika kumaliza machafuko nchini Syria yapo kwenye hata na inawezekana kabisa yasitekelezwe kutokana na hali ambayo inaendelea kushuhudiwa katika nchi hiyo.

Kellenberger licha ya kuona hatari ambayo ipo katika kutekeleza mapendekezo hayo sita lakini amesema ni lazima kila linalowezekana lifanyike ili kufikia malengo ambayo yamewekwa na Umoja wa Mataifa UN pamoja na Jumuiya ya Nchi za Kiarabu.

Hadi sasa jumla ya waangalizi thelathini wapo nchini Syria huku lengo likiwa ni kuongeza hadi wafike mia tatu na kuweza kufanya tathmini ya kina kubaini kile ambacho kinafanywa hasa maeneo ya Daraa, Homs na Hama ambako kunaonekana kama ngome ya upinzani.

Takwimu zinonesha kuwa watu zaidi ya mia tano wamepoteza maisha tangu serikali ya Damascus itangaze kusitisha mashambulizi dhidi ya wapinzani hatua ambayo ilifikiwa ili kutekeleza mapendekezo ya Mpatanishi wa Kimataifa Kofi Annan.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.