Serikali ya Senegal yampatia hifadhi ya kisiasa rais wa zamani wa Mali, Amadou Toumani Toure na familia yake
Rais aliyeondolewa madarakani nchini Mali kupitia Mapinduzi ya Kijeshi Amadou Toumani Toure amewasili nchini Senegal ambako ameomba hifadhi ya ukimbizi msemaji wa Rais Macky Sall, Abou Abel Thiam amethibitisha hilo.
Imechapishwa:
Toure amekimbilia Dakar kuomba nafasi ya ukimbizi kipindi hiki ambacho Utawala wa Kijeshi ukiwaachia wanasiasa na wanajeshi ambao waliwakamata mapema juma hili wakiwahusisha na serikali iliyoangushwa.
Watu hao ishirini na wawili wameachiwa kipindi hiki ambacho taifa hilo lipo chini ya serikali ya mpito ikiongozwa na Spika wa zamani wa Bunge Dioncounda Traore ikiendelea kujipanga kuhakikisha inarejesha utawala wa kidemokrasia katika nchi hiyo.
Jumuiya ya kimataifa iliweka shinikizo kwa serikali mpya ya Mali kuwaachilia huru wanajeshi na wanasiasa wanaoshikiliwa kwakuwa tayari utawala wa kidemokrasia umerejea nchini humo na sasa ni kuweka umoja wa kitaifa.
Wanajeshi wa Mali walikuwa wanamshikilia waziri mkuu wa zamani wa nchi hiyo pamoja na wanasiasa wengine kwa kile walichodai kuwa walichangia kwa kiasi kikubwa kwa rais Toure kushindwa kuwamudu wapiganaji wa kundi la Tuareg.
Serikali ya Senegal imethibitisha kumpokea kiongozi huyo na kukubali kumpa hifadhi kwa kile ilichoeleza kuwa ni kwaajili ya usalama wake na familia yake ambayo ilijikuta matatani baada ya kufanyika mapinduzi.