Syria yaongezewa muda zaidi na Umoja wa nchi za kiarabu kutia saini makubaliano ya amani
Jumuiya ya Nchi za Kiarabu imetoa muda usiozidi saa ishirini na nne kwa serikali ya Syria kuhakikisha inatekeleza maazimio ya kusitisha mauaji yanayotendeka katika nchi hiyo kinyume na hapo wataishushia vikwazo na kutaka ushirikiano kutoka Umoja wa Mataifa UN.
Imechapishwa:
Uamuzi huo umefikiwa baada ya Mawaziri wa Mambo ya Nje kutoka nchi wanachama kukutana jijini Cairo nchini Misri kujadili kile ambacho kinaendelea nchini Syria wakati huu ambapo wanaharakati wakisema watui hamsini wamepoteza maisha.
Jumuiya ya Nchi za Kiarabu umeutaka Umoja wa Mataifa UN kuwasaidia kwenye mpango huo wa kuhakikisha wanazima mauaji ambayo yanaendelea nchini Syria.
Katika maazimio ya Umoja wa nchi za Kiarabu yanaitaka Serikali ya Syria kuruhusu waangalizi wa kimataifa wa haki za binadamu kuingai nchini humo kufanya uchunguzi kuhusu tuhuma za maofisa wake kuhusika na mauaji ya kiholela dhidi ya raia ambao wanaipinga Serikali.
Siku ya Ijumaa ndio siku ya mwisho kwa Serikali ya Syria kutia saini makubaliano hayo au kukabiliwa na vikwazo vya kiuchumi ikiwemo kusitishwa kwa safari zote za ndege za kibiashara kuingia nchini humo pamoja na kuzifunga akaunti za benki kuu ya nchi hiyo katika nchi wanachama.
Wiki moja iliyopita waziri wa mambo ya nchi za nje wa Syria, Walid al-Muallem alisema kwamba Umoja huo umeiwekea nchi yake masharti ambayo ni magumu kutekelezeka na kwamba hatua ambazo zinataka kuchukuliwa na viongozi wa nchi wanachama ni kinyume cha katiba ya Umoja huo.
Hapo kesho viongozi hao watakutana mjini Cairo Misri kujadili hatua za kuchukua endapo nchi ya Syria itaendelea kushikilia msimamo wake.