Jeshi nchini Myanmar lasema litakabidhi madaraka kwa raia
Jeshi la Myanmar limesema tena, litapanga uchaguzi mpya na kuacha madaraka wakati huu maandamano yanapoendelea kushuhudiwa katika taifa hilo, kushinikiza kuachiliwa huru kwa kiongozi wa kiraia Aung San Suu Kyi.
Imechapishwa:
Msemaji wa Jeshi Brigedia Jenerali Zaw Min Tun amesema Jeshi liliamua kuchukua serikali kwa sababu ya wizi wa kura, kauli ambayo ameitoa bila ya ushahidi wowote.
Aidha, amesema kuwa shtaka la pili la jinai dhidi ya Aung San Suu Kyi, limefunguliwa dhidi ya kiongozi huyo.
Maandamano yamekuwa yakiendelea nchini humo tangu Februari tarehe 1 wakati jeshi lilipomkamata Aung San Suu Kyi baada ya chama chake kushinda idadi kubwa ya viti vya wabunge.
Wanajeshi wameendelea kushuhudiwa katika miji mbalimbali ya nchi hiyo kudhibiti waandamanaji wakati huu, Umoja wa Mataifa ukionya wanajeshi kuacha kuwashambulia waandamanaji na kujaribu kuzuia maandamano hayo.
Jeshi nchini humo limeamua kuzima mtandao wa Internet baada ya zaidi ya siku 10 za maandamano.