China: Mkosoaji mkubwa wa Xi Jinping ahukumiwa kifungo cha miaka 18 jela kwa ufisadi
Kiongozi wa zamani wa kampuni ya umma na mkosoaji mkubwa wa rais wa China Xi Jinping amehukumiwa kifungo cha miaka 18 kwa ufisadi, mahakama ya China imesema.
Imechapishwa:
Ren Zhiqiang, mwenyekiti wa zamani wa kampuni ya umma ya Huayuan, pia amepigwa faini ya yuan milioni 4.2 (takriban euro 525,960), Mahakama ya Beijing imesema kwenye wavuti yake.
Kulingana na ilani iliyotolewa Jumanne wiki hii, Ren Zhiqiang amerudisha mapato yote aliopata kinyume cha sheria, "amekiri kwa makosa yake," amekubali hukumu yake na hatakata rufaa.
Ren Zhiqiang alikamatwa mwezi Machi baada ya kumlinganisha rais Xi Jinping na mtu wa kuigiza wakati rais huyo wa China alikuwa akipongeza serikali yake jinsi inavyoshughulikia mgogoro wa kiafya unaosababishwa na virusi vya Corona.
Ren Zhiqiang alifukuzwa katika Chama cha Kikomunisti cha China mwezi Julai. Alishutumiwa mwezi huo huo matumizi mabaya ya pesa za serikali.