Serikali ya Myanmar yatoa onyo la kwanza kwa Aung San Suu Kyi
Mamlaka nchini Myanmar imemwandikia barua ya onyo kiongozi mkuu wa upinzani nchini humo Aung San Suu Kyi kuhusu chama chake kuendelea kujihusisha na shughuli za kisiasa.
Imechapishwa:
Kiongozi huyo ambaye aliachiliwa huru mwaka jana mwezi November amekuwa akishiriki mara kwa mara katika mikutano ya chama chake cha NLD hatua ambayo inaonekana kutaka kukijenga upya chama chake.
Waziri wa mambo ya ndani nchini humo amedhibitisha kumuandikia barua hiyo ya onyo kiongozi huyo pamoja na mwenyekiti wa chama chake kuwataka kusitisha mara moja harakati zozote za kisiasa ambazo chama hicho imekuwa ikizifanya siku za hivi karibuni.
Katika barua yake hiyo waziri huyo amekitaka chama hicho kusitisha harakati za kisiasa kwa sasa kama kweli kinataka kujenga demokrasia huru nchini humo.
Tangu kuachiliwa huru kwa mwanasiasa huyo, amekuwa akifanya mikutano kadhaa ya hadhara kuwashawishi wananchi kushinikiza mabadiliko zaidi nchini humo hali inayotishia kuzuka kwa machafuko nchini humo.
Utawala mpya wa nchi hiyo ulitangaza kusitisha harakati zote za kisiasa kwa vyama vya upinzani kwa wakati huu, mapaka pale nchi hiyo itakapokuwa kwenye chaguzi zake za kawaida kwa lengo la kuzuia machafuko.
Hili linakuwa ni onyo la kwanza kutolewa kwa utawala huo mpya ambao umesheheni wanajeshi wa zamani wa taifa hilo kutoa onyo kwa kiongozi huyo tangu aachiliwe huru.