Sudan Kusini imepokea idadi kubwa ya wakimbizi wanaotoka Sudan
Nairobi – Shirika la misaada katika Umoja wa mataifa limethibitisha kuwa Sudan Kusini imewapokea zaidi ya wakimbizi nusu milioni wanaotoroka mapigano katika nchi jirani ya Sudan.
Imechapishwa:
Katika ripoti yake ya hivi punde kuhusu mzozo wa Sudan, OCHA inasema watu 516,658 wamethibitishwa kuwasili nchini Sudan Kusini tangu kuzuka kwa mapigano tarehe 15 ya mwezi Aprili mwaka wa 2023.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, asilimia 81 ya watu waliongia nchini Sudan Kusini walikuwa wenyeji wa taifa hilo waliokuwa wakimbilia usalama wao nchini Sudan wakati asilimia 18 wakiwa ni wakimbizi wa Sudan.
Ocha pia imeeleza kuwa kulikuwa na ongezeko katika idadi ya raia wa Sudan waliosajiliwa kama waomba hifadhi jijini Juba mwezi huu.
Mapigano yamekuwa yakiendelea kuripotiwa nchini Sudan kati ya wanajeshi wa serikali na wapiganaji wa RSF, wito wa kimataifa wa kusitishwa wa makabiliano ukionekana kupuuzwa.