Kenya yaadhimisha miaka 60 ya uhuru kutoka kwa mkoloni Uingereza
NAIROBI – Rais William Ruto, ametumia maadhimisho ya miaka 60 ya uhuru wa nchi hiyo, kuwaambia Wakenya kuwa, Kenya inaelekea kujiondoa kwenye madeni, licha ya wananchi kuendelea kulalamikia kupanda kwa gharama ya maisha na kuongezewa kodi mbalimbali.
Imechapishwa:
Cheza - 00:55
Ruto ameeleza baadhi ya mafanikio ya nchi hiyo, baada ya kujitawala kwa miaka 60 sasa baada ya kupata uhuru kutoka kwa wakoloni, Waingereza.
Tumefanya maamuzi sahihi, wakati mwingine tukachukua maamuzi magumu na chungu sana, ili kuirejesha Kenya kutoka kwenye makali ya janga la dhiki ya madeni na kuipeleka nchi yetu katika mwelekeo mpya, amesema Ruto.
Kenya imekuwa ikikabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo mfumuko wa bei na kushuka kwa sarafu ambayo imesababisha gharama za ulipaji wa deni kupanda.
Rais Ruto ameendelea kusisitiza ahadi yake ya kuondoa viza kwa wageni wanaoingia nchini humo kuanzia Januari mwaka 2024.
'Uhuru wa Kenya'
Nchi hiyo ya Afrika Mashariki ilijinyakulia uhuru mnamo Disemba 12, mwaka 1963 kutoka kwa mkoloni wake Uingereza ambapo mamlaka ya kikoloni ya Uingereza iliwaweka kizuizini wanachama wa Mau Mau waliokuwa wakipigania uhuru, kutokana na muendelezo wa uasi kati ya mwaka 1952-1960.
Takriban watu 10,000 waliuawa huku makumi ya maelfu ya wengine wakizuiliwa bila kufunguliwa mashitaka katika kambi ambapo ripoti za kunyongwa, kuteswa na kupigwa kikatili zilikuwa za kawaida.