Juhudi za kumaliza mzozo wa Sudan zinaendelea
Nairobi – Muungano unaodai mabadiliko nchini Sudan, FFC, umeanzisha mawasiliano na pande zinazopigana nchini Sudan ili kupanga mkutano wa ana kwa ana katika siku zijazo, kujadili ramani ya njia ya kumaliza mzozo unaoisumbua nchi hiyo.
Imechapishwa:
Cheza - 00:42
Muungano huu umekuwa ukijihusisha kutoa shinikizo la kukomesha vita vilivyodumu kwa miezi minane, ambapo umekuwa ukiwakutanisha wanasiasa na asasi za kiraia na hivi karibuni walifikia makubaliano huko Addis Ababa kuunda kikosi kasi.
Taha Osman, mjumbe wa Ofisi ya Utendaji ya FFC, amewaambia waandishi wa habari kuwa, kufuatia mikutano ya mjini Cairo, muungano huo utawasilisha "ramani hiyo kwa jeshi na Vikosi vya RSF, akisisitiza kuwa hawafungamani na upande wowote kwenye mzozo huo.
Katika taarifa iliyotolewa baada ya kumalizika kwa mikutano hiyo, muungano huo ulitahadharisha kuhusu uwezekano wa vita hivyo kuchukua muda kumalizika, kutokana na mfululizo wa matukio ya hivi karibuni licha ya mazungumzo ya mjini Jeddah Saudi Arabia.
Haya yanajiri wakati huu UN ikikadiria kuwa raia zaidi ya 10,000 wa Sudan wameuawa tangu vita vilipozuka katikati ya mwezi wa Aprili, na zaidi ya milioni tano wameyakimbia makazi yao.