UN: Maelfu ya wakimbizi wa Sudan Kusini wako hatarini kukabiliwa na njaa
NAIROBI – Umoja wa mataifa umeonya asilimia 90 ya wakimbizi kutoka Sudan Kusini waliokuwa wamekimbilia Sudan na sasa wamelazimika kurudi nyumbani kufuatia mapigano wanakabiliwa na njaa.
Imechapishwa:
Cheza - 00:55
Shirika la mpango wa chakula duniani WFP, limesema mapigano yanayohusishwa na ugomvi kati ya kiongozi wa kijeshi jenerali Abdel Fattah al Burhan na aliyekuwa naibu wake na kiongozi wa kikosi cha RSF, Hamdan Dagalo, yamewalazimu wakimbizi karibu raia wa Sudan Kusini 300,000 kurejea nyumbani katika kipindi cha miezi 5.
Hata hivyo WFP imesema wengi wao wamelazimika kuishi bila chakula kwa siku kadhaa, asilimia 20 ya watoto wakiwa wameathirika na utapiamlo.
Mkurugenzi wa WFP jijini Juba, Mary-Ellen McGroarty, amesema inasikitisha kuwa wakimbizi hao waliokimbia hali hatari nchini Sudan sasa wamerudi kukutana na hali mbaya zaidi ya njaa.
Hali ya kibinadamu kwa wanaorejea haikubaliki na WFP inajitahidi kukidhi mahitaji ya kibinadamu yanayoongezeka mpakani, amesema McGroarty, akisema hakuna raslimali za kutoa msaada wa kuokoa maisha kwa wale wanaouhitaji zaidi.
Shirika la madaktari wasio na mipaka MSF, kwa upande wake, limeonya kuhusu ongezeko la visa vya magonjwa ya Malaria na Utapiamlo miongoni mwa wakimbizi wanaokimbia mapigano hayo.
Kwa mujibu wa takwimu za Benki ya Dunia, mmoja kati ya raia watano wa Sudan Kusini, wanaishi kwenye ufukara licha ya nchi hiyo kuwa na raslimali ya mafuta.