Kenya: Wanaharakati wa wanyama waomba kushiriki mazungumzo ya mabadiliko ya hali ya hewa
NAIROBI – Kuelekea mkutano wa mabadiliko ya tabia nchi barani Afrika wiki ijayo jijini Nairobi, wanaharakati wa kutetea masuala ya wanyama, wanataka suala la uharibifu wa mazingira, linalosababisha athari kwa mifugo kujadiliwa na kutafutiwa ufumbuzi.
Imechapishwa:
Wanaharakati hao wanasema ufugaji wa kisasa wa viwandani, mara nyingi haupewi kipaumbele kama chanzo cha mabadiliko ya hali ya hewa, katika sekta ya kilimo.
Mabadiliko ya hali ya hewa yanatudhuru kama binadamu, inadhuru wanyama wetu, pia mazingira na mazingira yakiharibika, wanyama huumia pia binadamu. Amesema Josiah Ojwang mtetezi wa wanyama.
Josiah Ojwang, mwanaharakati wa wanyama Kenya
Aidha, Victor Yamo mtaalam wa wanyama nchini Kenya, amesisitiza haja ya kuipa kipao mbele Ustawi wa Wanyama katika ajenda ya mkutano huo.
Tutanataka tuanze na Afrika Climate Week na Summit kwa sababu hapo ndio wajumbe wa kuenda COP 28 waanzia na tunataka ujumbe wetu ukuwe miongoni mwa masuala ambayo watajadili.
Victor Yamo, mtaalam wa wanyama, Kenya
Ukataji wa misitu kwa kiwango kikubwa, kwa ajili ya ufugaji wa idadi kubwa ya mifugo, umeonekana kuwa mojawapo ya uharibifu wa bayoanuai pamoja na chanzo cha magonjwa mapya ya mifugo na binadamu.
Tunafanya kazi na washikadau wa kimataifa ili wanyama wasipate kuathirika kutokana na mabadiliko haya ya tabia nchi. amesema Marryane Mwimali daktari wa mifugo nchini Kenya.
Marryane Mwimali,,ni daktari wa mifugo
Kenya itakuwa mwenyeji wa pamoja wa Mkutano wa Kwanza wa Hali ya Hewa ya Afrika kuanzia tarehe 4 hadi 6 Septemba 2023.Kauli mbiu ikiwa kujadili mabadiliko ya hali ya hewa,na maendeleo ya Afrika, na kuongeza uwekezaji barani.
Ripoti ya Victor Moturi, Nairobi, RFI Kiswahili.