Burkina Faso yaidhinisha sheria ya kuwatuma wanajeshi Niger
NAIROBI – Serikali ya Burkina Faso, imeidhinisha mswada unaoruhusu wanajeshi wake kutumwa kwenda nchi jirani ya Niger, ambayo inakabiliwa na tishio la kuvamiwa na wanajeshi wa ukanda wa ECOWAS, ili kurejesha utawala wa kiraia, baada ya mapinduzi ya mwezi Julai.
Imechapishwa:
Mswada huo uliidhinishwa kwenye kikao cha baraza la mawaziri cha utawala wa kijeshi siku ya Alhamisi, Agosti 31.
Licha ya kuidhinishwa, waziri wa ulinzi Kassoum Coulibaly hajaweka bayana undani wa mswada huo, lakini amesema tishio lolote la kiusalama katika nchi jirani ya Niger linaathiri usalama wa Burkina Faso.
Mswada huo sasa unasubiri kujadiliwa na kupitishwa hivi karibuni katika bunge la mpito.
Kiongozi wa utawala wa kijeshi nchini Niger jenerali Abdourahamane Tchiani, juma lilopita alisaini hati ya kuruhusu mataifa jirani kutoa msaada wa kijeshi iwapo ECOWAS itafanya kweli tishio la kutumia wanajeshi kushinikiza kurejeshwa madarakani rais aliyepinduliwa Mohammed Bazoum mnamo Julai 26.
Baadaya mapinduzi jeshi la Niger liliungwa mkono na nchi jirani za Mali na Burkina Faso, ambazo marais wake pia walipinduliwa kwa madai kuwa walifeli kukabiliana na wanajihadi ambao wamedunisha usalama katika eneo la Sahel.